MAJIKO SANIFU YA KISASA (UKOMBOZI)Kwa muda wa miaka minane ambayo WUWE imekuwa ikifanya kazi yake, imekuwa ikitengeneza majiko sanifu ya kuni yanayofahamika sana kwa jina la "Ukombozi". Jiko hili la ukombozi, limepewa jina hilo kutokana na kumkomboa mwanamke katika kazi ya kutafuta kuni mara kwa mara. Jiko hili linatumia kuni chache sana, ukilinganisha na jiko la majifya matatu, ambalo ni maarufu kwa maeneo mengi ya Tanzania.
Dr Mary wa kituo cha Afya Ruanda, katika wilaya ya Mbozi mkoani Mbeya anasema "Tangu nimejengewa jiko la Ukombozi, limenipunguzia sana matumizi ya kuni". Anaeleza zaidi kwa kusema, "Kabla ya kuwa na jiko hili, nilikuwa natumia kuni za shilingi 2000 kwa wiki, lakini baada ya kujengewa jiko hili na Mama Mmbaga mwaka 2001, kwa sasa natumia kuni zisizogharimu zaidi ya shilingi 1000 kwa wiki" Maelezo kama haya pia yanatolewa na Mama Fatma Mkangama wa kijiji cha Umwe Kati, wilayani Rufiji, katika mkoa wa Pwani. Huyu naye ni kati ya watu waliojengewa majiko haya maarufu ya Ukombozi.
Kimsingi, jiko la ukombozi hutengenezwa kwa teknolojia rahisi, lakini iliyo makini sana. Jiko hili hutengenezwa kwa kutumia mchanganyiko maalum wa udongo wa kichuguu, samadi mbichi, maji na majani maalumu yanayoteleza, kwa kutumia vipimo maalum. Bidhaa hizi kuchanganywa na kufinyangwa pamoja na kufanya mchangayiko mgumu. Mseto huu ndio hutumika kujenga jiko hili. Baada ya jiko kujengwa, huwa tayari kwa matumizi baada ya kukauka kwa wiki mbili.
WUWE inaendelea kusambaza teknolojia hii kwa kasi katika mikoa mbali mbali. Mikoa ambayo imeshafaidi teknolojia hii ni Morogoro, Pwani, Tanga, Mbeya, Kagera, Kilimanjaro, Manyara na Arusha. Malengo ya taasisi hii ni kusambaza teknolojia hii kwa Tanzania nzima.
Pichani: Mafundi wa WUWE wakijenga jiko la Ukombozi